WANANCHI wa Kijiji cha Nyashimba katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu mkoani Mwanza wameushukuru uongozi wa hamshauri hiyo kwa kuwajengea zahanati ya pamoja na shule ya sekondari hali itakayochochea maendeleo ya sekta ya afya na elimu kijijini hapo.
Hayo yamebainishwa jana Alhamisi tarehe 12 Juni 2025 katika ziara ya Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Simon Mpandalume ambaye pia ni Diwani wa kata ya Nyigogo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi wananchi hao akiwamo Elizabeth Komba amesema ujenzi wa zahanati hiyo utakuwa mkombozi kwa wakati wa Kijiji hicho hasa ikizingatiwa wakazi wake walikuwa wanatembea umbali mrefu kufuata huduma katika hospitali ya wilaya.
“Lakini zahanati hii ikikamilika hakika akina mama hawatapa tena shida ya kujifungua kwani huduma watapata hapa na hata baada ya muda tunatarajia itapandishwa hadhi kuwa kituo cha afya.
“Kuhusu shule ya sekondari Nyashimba pia itawasaidia Watoto wetu kuepukana na vishawishi mbalimbali walivyokuwa wanakumbana navyo pindi wanapoenda shule jirani za Kinango,” amesema Elizabeth na kuungwa mkono na Mchunga Hernest Cherehani ambaye amesema ujio wa miradi hiyo imekuwa chachu kwa wananchi kuendelea kuhamasisha kuchangia miradi ya maendeleo.
Awali akizungumza na wananchi hao na kuwashukuru kwa kumpa nafasi ya kuwaongoza kwa miaka mitano, Mpandalume amesema miradi hiyo inatekelezwa kwa mapato ya ndani ya halmashauri pamoja na nguvu za wadau akiwamo mbunge wa Magu, Boniventura Kiswaga.
Amesema zahanati hiyo ambayo ilianza kujengwa mwaka 2020, imetumia zaidi ya Sh milioni 45 fedha za mapato ya ndani ya halmashauri huku mbunge akichangia saruji mifuko 150.
Aidha, ameahidi kumalizia ujenzi wa zahanati hiyo ambapo halmashauri itatoa tena Sh milioni 35 ambapo hadi kufikia Agosti mwaka huu ujenzi huo utakamilika na mradi kuzinduliwa na kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru.
Kwa upande wa mradi wa shule ya sekondari tayari ulioanza 2020/2021 hadi sasa umefikia hatua nzuri huku kazi iliyobaki ikiwa ni kukamilisha ujenzi wa vyoo.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa