KATIKA kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi na kuhifadhi mazingira, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania katika wilaya ya Magu, umezalisha na kugawa miche ya miti aina tofauti zaidi ya 200,000 kwa wananchi na makundi mbalimbali wilayani huyo.
Pia katika kuadhimisha wiki ya mazingira duniani ambayo kilele chake kinafikiwa tarehe 5 Juni mwaka huu, TFS – Magu imegawa miche ya miti 250 kwa wananchi na shule mbalimbali wilayani humo kwa ajili ya kupanda miti ya kivuli na mtunda na kufikisha idadi ya miche 200,250 iliyogawiwa hadi sasa.
Hayo yamebainishwa leo Jumatano tarehe 4 Juni, 2025 na Afisa uhifadhi misitu II kutoka TFS Magu, Marwa Mshehe wakati akizungumza katika maadhimisho ya siku ya mazingira yaliyofanyika wilayani humo.
Mshehe amesema katika kipindi cha mwaka mmoja tayari wamegawa miche hiyo ya miti kwa makundi mbalimbali ambayo wanaamini imekwenda kuongeza uoto wa asili katika eneo hilo huku jamii ikifaidika kutokana na miche ya miti ya matunda iliyogawiwa pia.
Naye Balozi wa Mazingira Tanzania kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, Ahidi Sinene ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimishi hayo ameupongeza uongozi wa wilaya hiyo kwa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha wananchi kupanda miti na kuhifadhi mazingira.
“Tupo kwenye wiki ya mazingira duniani, maadhimisho yake ni tarehe 5 Juni kila mwaka, kwa hiyo ofisi ya Makamu wa Rais tunapita kwa wananchi kuwahasisha kupinga matumizi ya plastiki kwa sababu kwanza ni sumu, ukiitumia binafsi unaenda kufanyiwa operesheni, lakini inaharibu ikolojia ya maji na kudumaza mazao, tunapaswa kupinga matumizi ya plastiki na kutumia mifuko ambayo ni rafiki kwa mazingira yetu,” amesema.
Naye Katibu Tawala wa wilaya hiyo ya Magu, Jubilate Lawuo amesema katika maadhimisho hayo ambayo wamegawa miche ziadi ya 100 kwa wananchi wa shule ya msingi Nyalikungu, Magu imeendelea kuwa mfano wa kuigwa katika kutekeleza mpango wa Rais Samia wa kwa kuwa balozi bora wa mazingira.
“Rais Samia amekuwa balozi wa kwanza katika kuboresha mazingira. Katika kipindi cha miaka mitano amehamasisha wananchi kuachana na kutumia nishati safi na sisi Magu tumefanikiwa kuvutia wadau ambao wamesambaza mitungi ya gesi zaidi ya 3900 kwa akina mama ntilie na watu wa makundi mengine ili waachane na matumizi ya mkaa.
“Nami nimekuwa mstari wa mbele kuadhimishwa siku hii kwa kupanda miti ili kuhamasisha wananchi waendelee kuachana na mkaa ili kuendana na kuli mbiu yam waka huu inayosema “Mazingira yetu na Tanzania ijayo, tudhibiti matumizi ya plastiki,” amesema.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa