ILI kuendana na mabadiliko ya mitaala ya elimu ya msingi na awali, Halmashauri ya wilaya ya Magu imegawa zana za ujifunzaji na ufundishaji kwa shule za msingi 53 za serikali zenye madarasa ya awali wilayani humo.
Zana hizo zenye thamani ya Sh milioni 34, zimetengenezwa kwa ufadhili wa mradi wa BOOST ambao ni mradi wa kuimarisha na kuboresha elimu ya awali na msingi.
Akigawa zana hizo leo Alhamisi tarehe 5 Juni, 2025 katika Kituo cha Walimu TRC Nyalikungu wilayani Magu mkoani Mwanza, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Mohamed Ramadhani amewaonya walimu wa shule zilizopokea zana hizo kutozifungia stoo kwa dhana kuwa wanafunzi wataziharibu.
“Mwaka juzi tulitoa kwa shule 28, mwaka huu tumetoa kwa shule 53 lakini Magu tuna shule 111 za serikali, sasa ifike mahali mtoto wa chekechea anayetoka palipo na zana hizi awe na utofauti lakini naamini pia wasiopata wataenda kuiga mfano huu kuzitengeneza kwa wingi zaidi.
“Naishukuru serikali kwa jitihada kubwa inazofanya na wizara ya elimu kwa sababu inakuja na bunifu mbalimbali kuhakikisha watanzania na watoto wetu wanaenda na mabadiliko ya ufundisha, zamani ilikuwa tunaumba herufi kwenye mchanga sasa zana zipo, tunaweza kuiga kama dunia ya kwanza walipo,” amesema na kuongeza;
“Mwalimu wangu tunakutegemea sana kuhakikisha hiki kitu kinaingia katika ufahamu wa mtoto. Mnafahamu kabisa kuwa kwenye sera ya elimu tutakuwa na elimu ya ufundi stadi ili mtoto akimaliza kidato cha nne awe na ujuzi wa kiufundi kama ni wa magari au umeme.
“Kwa hiyo mwalimu jitahidi hiki ambacho utakipokea kahakikishe kinaenda kuingia kwenye uelewa wa mtoto, kisiende kufungiwa staff… badala ya kufungiwa stoo ili visipotee, wafundisheni watoto namna ya kuvitumia na kuvitunza ili wasiviharibu kwa sababu pamoja na utundu wao wana uelewa hivyo nina uhakika watavitunza,” amesema.
Naye Mwalimu Jackson Buhatwa ambaye ni Kaimu Afisa Elimu Msingi Magu, amesema zana hizo za kufundishia kwa wanafunzi wa darasa la awali, zimetengenezwa na walimu wenyewe kwenye kituo cha TRC - Nyalikungu.
“Tuna jumla ya shule 111 za serikali lakini awamu hii ya pili ni shule 53 zimefaidika na mradi huu. Kila shule imepata Sh 6045,500 kwa ajili ya utengenezaji wa zana ambazo zitatumika kufundishia wanafunzi wa awali.
“Tunaipongeza serikali kwa kufanikisha upatikanaji wa zana hizi ili kupunguza changamoto kubwa ya KKK, wanafunzi wetu wana changamoto kubwa kutokujua stadi hizi tatu kusoma, kuandika na kuhesabu. Msaada huu umetia chachu kwa walimu na wanafunzi wetu ili kupunguza janga kubwa la wanafunzi kutojua hizi stadi tatu.
“Niwapongeze walimu walioshiriki zoezi hili la utengenezaji, hizi zana na huu ni mwanzo, kwani wana uwezo wa kuzitengeneza na kuambukiza wenzao ambao hawakupata zana hizi. Tunamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutukumbuka,” amesema.
Aidha, Mwalimu kutoka shule ya msingi Itumbili iliyopo wilaya ya Magu, Marry Shigela ameeleza fuaraha yake kupokea vifaa hivyo kwani vitamsaidia kurahisisha ufundishaji kwa wanafunzi wa darasa la awali ambao watapokea maarifa au watajifunza kwa kuona na kugusa.
“Tulikuwa na changamoto nyingi kuhusu zana za ufundishaji kwa sababu mwanafunzi ilikuwa haoni zaidi ya kile kinachoandikwa ubaoni lakini sasa ataona na watoto watapokea maarifa, tunaahidi tutafanya juhudi ili watoto waende kupokea maarifa kupitia vifaa hivi,” amesema.
Naye Daniel Joseph - mwalimu shule ya msingi Mwabui, amesema zana hizo zitamsaidia mtoto kupata uelewa zaidi, kumfanya aipende shule hasa ikizingatiwa watoto wadogo hujifunza kwa vitu anavyoviona.
“Kutokana na mabadiliko ya mitaala zana hizi zitasaidia sana makuzi ya mtoto kuendana na wakati. Tunaahidi kufanya kazi kwa bidi lakini pia zana zitatumika ipasavyo kwa watoto, tutaenda kusimamia badala ya kuwa kama pambo,” amesema.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa