ZAIDI ya watumishi 300 ambao ni walimu wakuu, walimu wa ununuzi, watendaji wa kata na wa vijiji katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu wamepewa mafunzo kuhusu usimamizi na ununuzi wa umma kielektroniki (NeST), ili waelewe namna ya kuomba zabuni, kusaini mikataba na kuitekeleza.
Mafunzo hayo yanayotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), yanafanyika katika ofisi za Halmashauri ya wilaya Magu mkoani Mwanza kwa siku tatu kuanzia Mei 26 hadi 28, 2025.
Mafunzo hayo pia yanahusisha wazabuni na maofisa ununuzi kutoka idara za ununuzi ya halmashauri ya Magu.
Akizungumza kwenye mafunzo hayo, Afisa Ununuzi Mwandamizi wa PPRA kanda ya Ziwa, Evaristo Mtilega, amesema kuwa licha ya mfumo huo kuanza kufanya kazi tangu 2023, sasa kinachoendelea ni kuuboresha na kuongeza moduli mpya zitakazoongeza ufanisi wa utekelezaji wa ununuzi wa umma nchini.
Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Idara ya Manunuzi, Hilda Mwangamila amewataka wadau hao ununuzi kutumia mfumo wa NeST ipasavyo ili kusaidia kupata wazabuni wenye gharama zinazolingana na thamani ya fedha zinazolipwa.
Aidha, amewataka walimu hao na watendaji kuzingatia muongozo mpya wa ununuzi kwa sababu umeongeza uwazi.
"Mfumo huu wa kielektroniki umeundwa ili kuboresha uwazi, ushindani na usawa katika michakato ya manunuzi ya umma, hivyo tunaamini kwa mafunzo haya yatasaidia kutatua changamoto hususani kuharakisha michakato ya manunuzi ya vifaa vya ujenzi na upatikanaji wa mafundi kwani mfumo ni rafiki na kufanikisha miradi ya maendeleo kumalizika kwa wakati,” amesema na kuongeza;
“Ukiona umekosea usisite kuja ofisini kwetu kupata maelekezo kwa sababu ninyi ni sisi na sisi ni ninyi… milango ipo wazi, ninaamini waliopita kwenye mikono yangu wamepata maelekezo mazuri.
“Pia tumekubaliana wote kama kitengo kwamba jukumu letu la kwanza mpaka la tatu ni kuwahudumia ninyi vizuri ili documents zenu zikae vizuri. Kuna hoja za risiti nataka niwaase kuwa wazabuni sio ndugu zetu, mnapokuja kulipa hakikisha umeambatanisha na risiti kwani lengo sio kuwakomoa… ni kuhakikisha umeondokana na hoja za risiti. Kwa hiyo usimpe malipo kabla ya kukupa risiti. Hoja zinatesa, tukubaliane wote kwa pamoja kufuta hoja za manunuzi,” amesema Mwangamila.
Naye mmoja wa walimu walioshiriki mafunzo hayo, Hyahasisi Husein Msigala ambaye ni mwalimu wa ununuzi katika shule ya msingi Busekwa iliyopo kata ya Bujashi amesema mafunzo hayo yamewaongezea mbinu ya kusimama miradi ya maendeleo kwa uzalendo.
Amesema miongoni mwa mafunzo waliyofundishwa ni namna ya kufanya majadiliano kati ya mzabuni na taasisi za ununuzi ili kuweka vizuri makubaliano katika mkataba utakaokuja kusainiwa.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa