Walimu wenye mahitaji maalumu katika Halmashauri ya wilaya ya Magu wamekabidhiwa vifaa saidizi kwa lengo la kuboresha mbinu za ufundishaji na kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu.
Vifaa hivyo kutoka Serikali kuu vimekabidhiwa kwa walimu watatu wenye mahitaji maalum kutoka shule za msingi za Magu, Nenge pamoja na shule ya sekondari Moha.

Akikabidhi vifaa hivyo leo Februari 4, 2026 wilayani Magu kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Mkuu wa Idara ya utumishi, Henry Sadatale amesema vifaa vilivyotolewa ni kompyuta mpakato (laptop) tatu.
Amesema kuwa vifaa hivyo vitawawezesha walimu kutumia teknolojia katika ufundishaji, hivyo kuchangia ongezeko la ufaulu kwa wanafunzi.
Aidha, amewataka walimu hao kuvitunza na kuvitumia kwa malengo yaliyokusudiwa ili kuleta tija iliyokusudiwa na Serikali.
“Pia niishukuru wizara kwa kuendelea kuratibu zoezi hili kwani hata sisi inatusaidia kufuatilia utendaji kazi wa walimu wetu,” amesema.

Akizungumza kwa niaba ya walimu wenzake waliopokea vifaa hivyo Aloyce Masero (Moha Sekondari), ameishukuru Serikali kwa kuwapatia vifaa saidizi ambavyo vitawarahisishia kazi ya ufundishaji, hasa katika matumizi ya teknolojia, ikilinganishwa na awali ambapo walikuwa wanategemea vitabu pekee.
Walimu wengine waliopatiwa vifaa hivyo ni Sabare Mseti kutoka shule ya msingi Magu na Lameck Edward kutoka shule ya msingi Nenge.
Ikumbukwe kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alizindua zoezi la ugawaji wa vifaa vya kielimu na vya saidizi kwa walimu, wakufunzi na walimu tarajali wenye ulemavu vyenye thamani ya shilingi bilioni 5.3 nchini kote.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa