KATIKA kuchagiza maendeleo kwa wananchi wa Magu mkoani Mwanza, Mbunge wa jimbo hilo, Boniventure Kiswaga amegawa mifuko 1,040 ya saruji kusaidia ujenzi wa maabara, madarasa na zahanati katika kata 12 zilizopo katika jimboni humo.
Pia amegawa madawati 130 kwa shule mbalimbali za msingi na sekondari sambamba na vifaa mbalimbali vya upauaji wa nyumba za walimu, shule na zahati zinazoendelea kujengwa katika jimbo hilo.
Saruji na vifaa hivyo vimekabidhiwa na wajumbe wa kamati ya mfuko wa jimbo walioongozwa na Lucas Bomoa ambaye ni Diwani wa Kandawe (CCM), kwa niaba ya Kiswaga kwa lengo la kuendeleza ujenzi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa jimboni humo.
Akizungumza na wananchi wa kata hizo jana Alhamisi na leo Ijumaa katika ziara maalumu ya kukabidhi vifaa hivyo, Bomoa amesema Kiswaga amedhamiria kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya elimu na afya jimboni humo ili kustawisha maendeleo ya wananchi wake.
Akipokea misaada hiyo, baadhi ya walimu wakuu wa shule za msingi na sekondari akiwamo Mwalimu Mkuu shule ya Msingi Lutale, Hezron Kitundu amemshukuru mbunge huyo kwa kusaidia vifaa vya upauaji wa nyumba ya walimu.
“Tunashukuru sana kwa sababu baada ya nyumba hii kukamilika walimu tutakaa karibu na shule na kufuatilia kwa karibu maendeleo ya wanafunzi wetu,” amesema.
Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Deleli iliyopo kata ya Bujashi, Leticia Mlomo amemshukuru mbunge huyo kwa kuwapatia mifuko 100 ya saruji ambayo inakwenda kusaidia ujenzi wa maabara.
“Hitaji letu kubwa ni maabara kwa sababu sasa tumepata kidato cha tatu. Tunaahidi kutumia vema msaada huu ili kuhakikisha inatumika kama inavyotakikana kwenye ujenzi,” amesema.
Wakati Elias Petro - mwenyekiti Kijiji cha Ihushi ambaye amepokea mifuko 100 ya saruji pia ameahidi kuisimamia katika ujenzi wa mradi ulioanzishwa na wananchi wake.
Hakimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Haki zote zimehifadhiwa